Maoni Ya Wateja

Wizara Ya Afya

WATAALAMU WA VINASABA TUMIENI TEKNOLOJIA,WELEDI UWE KIPAUMBELE KWENYE MAJUKUMU YENU: DKT. JINGU

Posted on: May 6th, 2024



Na WAF, Dodoma

Katibu Mkuu wa Wizara ya Afya, Dkt. John Jingu, ametoa rai kwa kamati ya kitaalamu wanaofanya uchunguzi wa Vinasaba vya Binadamu kuzingatia matumizi ya teknolojia huku wakizingatia weledi na kufuata maadili ya kazi ili kuepuka madhara au migogoro inayoweza kujitokeza.

Dkt. Jingu amesema hayo leo 6 Mei, 2024 jijini Dodoma wakati akizindua Kamati ya kitaalamu ya Vinasaba vya Binadamu ikiwa ni sehemu ya utekelezaji wa Sheria ya Vinasaba vya Binadamu Sura ya 73 inayo ongozwa na Mwenyekiti wake ambaye pia ni Mganga Mkuu wa Serikali Prof. Tumaini Nagu.

Katibu Mkuu Dkt. Jingu amesema serikali ina imani na kamati hiyo kwani itasaidia Mamlaka ya Maabara ya Mkemia Mkuu wa Serikali kutimiza wajibu wake kwa nchi na Serikali na kuendeleza mahusiano mema na Taasisi ambazo zina majukumu yanayoshabihiana.

“Ni matumani yangu kuwa kamati tunayoizindua hii leo itasaidia Mamlaka ya Maabara ya Mkemia Mkuu wa Serikali kutimiza wajibu wake kwa nchi na Serikali, lakini pia itaendeleza mahusiano mema ya kiutendaji kati ya Mamlaka hii na taasisi ambazo zina majukumu yanayoshabihiana”. Amesema Dkt Jingu.

Katibu Mkuu huyo ameongeza kuwa, Masuala ya Vinasaba yana mambo mengi ambayo yanaweza kuisaidia jamii, lakini pia yanahitaji kiwango kikubwa cha kimaadili na kiusimamizi, hivyo amewataka wataalam kufanya kazi kwa weledi na kwenda sambamba na mabadiliko ya teknolojia ya vinasaba kwa kuwa dunia inabadilika kwa haraka kila siku.

Kwa upande wake Mkemia Mkuu wa Serikali Dkt. Fidelice Mafumiko, ametaja majukumu ya msingi yanayofanywa na Mamlaka ikiwemo sheria ya Udhibiti Matumizi ya Vinasaba vya Binadamu sura ya 73.